NEMC YAFANYA MKUTANO NA WAANDISHI WA HABARI KUTOA TAARIFA MAALUMU YA KUDHIBITI KELELE CHAFUZI NA MITETEMO


Bazara la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limezifungia baa na kumbi za starehe 89 katika mikoa mitatu ikiwemo Mkoa wa Dar es salaam, Mwanza na Dodoma kwa kupiga kelele zinazozidi viwango kinyume cha sheria ya mazingira ya mwaka 2014.

Akizungumza Jijini Dar es salaam kwenye kikao cha mrejesho wa operesheni ya msako wa kubaini baa na kumbi za starehe zinazopiga kelele zilizozidi viwango, Mkurugenzi Mkuu NEMC Dkt.Samuel Gwamaka amesema wamefikia hatua hiyo kutokana na maeneo hayo ya biashara kupiga kelele na mitetemo iliyozidi viwango.

Amesema mpaka wamefikia uamuzi huo wa kuwafungia ni kwa sababu sio mara ya kwanza kwa kumbi hizo kufanya makosa hayo, licha ya NEMC kuwaonya kwa nyakati tofauti lakini hawakuweza kufuata utaratibu.

"Hatupendi kufungia kazi zenu lakini inatupasa tufanye hivyo kama hamuwezi kufuata utaratibu uliowekwa, tunajua mnalipa kodi pia mmetoa ajira kwa vijana lakini mnapovunja sheria na utaratibu lazima tuwachukulie hatua". Amesema Dkt.Gwamaka

Hadi sasa Baraza hilo limezifungia baa na nyumba za starehe 89 Jijini Dar es salaam, tano Dodoma sita katika mkoa wa Mwanza na kuweka masharti matatu ikiwemo kufunga vifaa vya kudhibiti kelele na kulipa faini ya milioni tano kwa wale waliowahi kuonywa na milioni mbili wa wafanyabiashara wapya.