NEMC YAFUNGIA KIWANDA CHA AMIGO -KIGAMBONI


Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC limekifungia kiwanda cha kutengeneza maturubai cha AMIGO kilichopo Mtaa wa Kichangani, Kata ya Kisarawe 11 Wilaya ya Kigamboni kwa kutumia mifuko ya plastiki isiyokidhi viwango kufungashia bidhaa zao.

Zoezi hilo limefanyika leo wakati wa ziara ya ukaguzi wa utekelezaji wa katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki kama kifungashio kwenye masoko na viwandani kilichohusisha wajumbe kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC.

Akizungumza katika ziara hiyo Bi. Liliani John ambaye ni Meneja wa Kanda ya Kusini Mashariki (NEMC) amesema kiwanda hiki kimekiuka Kanuni za Usimamizi wa Mazingira za kupiga marufuku mifuko ya plastiki za mwaka 2022 kwa kutumia mifuko ya Plastiki kama kifungashio cha bidhaa yao.

Amesema ‘Serikali imeshatoa maelekezo ya namna sahihi ya matumizi ya mifuko mbadala. Mifuko ya plastiki inatumika kwa zile bidhaa za viwandani zilizopewa msamaha ambazo zisipohifadhiwa zinapoteza ubora wake kama vile dawa n.k’ amesema Bi liliani John.

Ameongeza kuwa kwa ile mifuko ya plastiki inayotengenezwa kwa ajili ya kuhifadhi ubora wa bidhaa za viwandani ni lazima ikidhi vigezo ikiwemo nembo ya tbs, jina la mtengenezaji, lakiri au alama inayotambulisha bidhaa iliyofungashwa kabla ya kuuzwa au kusambazwa.