​NEMC YATOA HUDUMA ZA USAJILI WA MIRADI PAMOJA NA WASHAURI ELEKEZI WA MAZINGIRA KWA NJIA YA MTANDAO


Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeendelea kutoa huduma ya usajili wa washauri elekezi wa mazingira pamoja na usajili wa miradi katika maonesho ya Kimataifa ya wakulima Nanenane yanayoendelea Mkoani Mbeya.

Akitoa huduma hiyo kwa njia ya mtandao kwa wadau wa Mazingira, Bi Suzan Chawe ambaye ni Afisa Elimu Jamii mwandamizi wa Baraza, amesema huduma hii ni fursa kwa wadau wetu wanaohitaji cheti cha mazingira na usajili wa ushauri elekezi kwani inarahisisha mchakato mzima wa upatikanaji wa cheti kinachompa fursa ya kutekeleza majukumu yake kisheria.

Amesema Baraza linasimamia miradi inayofanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) kwa njia ya mtandao kupitia (eia.nemc.or.tz) kwani njia hii inamuwezesha mwekezaji kuanzisha mchakato wa (TAM) au ukaguzi wa Mazingira (EA) kupitia mfumo wa usimamizi wa mradi (PMS)

Ameongeza kuwa katika kusajili miradi mwekezaji anatakiwa kufungua akaunti yake, kuchagua mshauri elekezi, kujaza fomu ya usajili, kufanya uchunguzi wa kina pamoja na Baraza kufanya mapitio ya taarifa za miradi.

Nyingine ni msahuri elelekezi kuwasilisha andiko lililoboreshwa kwa Baraza, Baraza kuwasilisha mapendekezo ya mradi kwa Mhe.Waziri mwenye dhamana ya mazingira, kuidhinishwa kwa ripoti ya TAM na hatua ya mwisho ni kuidhinishwa kwa mradi.

Aidha amezitaja faida za kusajiliwa kwa njia ya mtandao kuwa ni kuongeza ufanisi, kupata taarifa sahihi kutoka kwa wataalamu wa mazingira, kuboresha utunzaji kumbukumbu, kuwezesha utengano wa majukumu kati ya mshauri mwelekezi na mwekezaji pamoja na kuboresha ukusanyaji wa ada.

Karibu Banda la NEMC maonesho yaNanenane tukuhudumie kidigitali