​NEMC PAMOJA NA JMAT WAANDAA KONGAMANO KWA VIONGOZI WA DINI KUHUSU ATHARI ZA SAUTI ZILIZOZIDI VIWANGO KATIKA NYUMBA ZA IBADA


NEMC PAMOJA NA JMAT WAANDAA KONGAMANO KWA VIONGOZI WA DINI KUHUSU ATHARI ZA SAUTI ZILIZOZIDI VIWANGO KATIKA NYUMBA ZA IBADA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira(NEMC) kwa kushirikiana na Jumuia ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT) wameandaa kongamano la Kitaifa la Kujenga uelewa kuhusu athari zitokanazo na sauti zilizozidi viwango katika nyumba za ibada litakalofanyika Juni 12, 2023 Jijini Dar es salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Mwenyekiti Taifa Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT), Sheikh Dkt. Alhad Issa Salum amesema Kongamano hilo linalotarajiwa kuhudhuriwa na viongozi wa vyama na Serikali limelenga kujenga uelewa juu ya sauti zilizodi viwango katika nyumba za ibada ili kwa pamoja upatikane muafaka wa namna yakuenenda katika kudhibiti sauti zilizozidi viwango kwa msatakabali mzima wa Mazingira kwa maendeleo endelevu ya Taifa.

Shekh. Salumu amesema Mgeni rasmi katika kongamano hilo anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Kassim Majaliwa na kuwataka viongozi wote wa dini na madhehebu kuhudhuria ili kuweza kupata fursa ya kuelewa athari zitokanazo na sauti zilizozidi viwango.

‘Leo tumewaita kwa jambo moja kubwa linalohusiana na mstakabali na umuhimu wa mazingira yetu Nchini, Jambo hili linahusiana na kongamano kubwa lililoandaliwa na (NEMC) pamoja na (JMAT), tumeandaa kongamano hili linalotarajiwa kufanyika siku ya Jumatatu, katika ukumbi wa JNICC kwa lengo la kupata elimu na uelewa juu ya sauti zilizodizi viwango na athari katika mazingira.’ Amesema Sheikh.

Ameongeza kuwa Kongamano hilo litawajengea uelelewa zaidi katika lile linalokusudiwa na kupeleka waumini na wananchi wote kuishi kwa Amani na utulivu na kuainisha mada kuu mbili zitakazojadiliwa kuwa ni utiifu kwa mamlaka kwa mujibu wa biblia na Qur’an na sunna.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt Samuel Gwamaka amesema kwa kipindi hiki wamewalenga hasa viongozi wa dini pamoja na viongozi wa kimila hivyo amewataka wafike ili kuwapatia elimu itakayowaandaa kuwa mabalozi wazuri wa mazingira kwa watu wanaowaongoza.

Tunaamini kwamba kwa kutoka elimu hii inayohusiana na suala la mazingira katika maeneo mbalimbali inayogusa jamii hasa kwenye masuala ya kiafya, viongozi hawa watakuwa mabalozi wazuri kufikisha elimu hiyo kwa wale ambao wanawalea katika nidhamu’ Amesema Dkt. Gwamaka.