​WAZIRI JAFO AZINDUA MWONGOZO WA UKAGUZI WA MAZINGIRA MIRADI YA UJENZI


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo amezindua Mwongozo wa Ukaguzi wa Mazingira kwa miradi ya ujenzi ulioandaliwa na NEMC kwa kushirikiana na Kituo cha Sayansi na Mazingira cha Nchini India (CSE),

Akizindua Mwongozo huo jijini Dodoma ulioipa NEMC mamlaka ya kuhakikisha hali ya mazingira nchini inaboreshwa hasa mazingira ya uwekezaji, Dkt. Jafo amesema Mwongozo huo umezingatia mahitaji halisi ya Nchi ikiwemo ukuaji wa Miji na majiji hasa ikizingatiwa suala zima la Uhifadhi na Usimamizi wa mazingira ni mojawapo ya maeneo ya vipaumbele vilivyopo katika malengo makuu ya Serikali.

Mhe. Dkt. Jafo amesema Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kama chombo chenye dhamana ya mazingira linao wajibu wa kuongeza wigo wa uandaaji miongozo ya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) kupitia sekta za viwanda, nishati, kilimo na maji ili kuharakisha zoezi la mapitio ya miradi inayohitaji ufanyaji wa Tathimini ya Athari kwa Mazingira.

‘’Kipengele Na. 17 cha Makubaliano ya Mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu Maendeleo Endelevu unazitaka nchi wanachama kuhusisha Tathmini ya Athari kwa Mazingira katika miradi ambayo inasababisha madhara kimazingira, katika kutekeleza kipengele hicho zilianzisha taasisi na kutengeneza Sera na Sheria ikiwa ni pamoja na Kanuni kama ilivyo kwenye Kanuni ya Athari ya Mazingira za Mwaka 2005 na zile za Mwaka 2018’’ amesema Dkt. Jafo.

Waziri Jafo ameongeza kuwa Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) hufanyika ili kuweka mifumo bora ya kulinda mazingira ikiwa ni pamoja na kupunguza kiwango cha taka zinazozalishwa, kutoa kipaumbele katika masuala ya jamii, kuainisha athari zilizopo na madhara yanayoweza jitokeza kutokana na miradi inayoanzishwa.

Amebainisha kuwa NEMC inapokea zaidi ya miradi 2000 kwa mwaka kwa ajili ya mapitio na kuongeza kuwa idadi hiyo ya miradi ni kubwa na itaweza kupitiwa kwa ufanisi iwapo kutakuwa na miongozo ya kila sekta kama inavyoelekezwa katika Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004.

Dkt. Jafo ameishukuru Serikali ya India kupitia kituo hicho kwa kushirikiana na NEMC katika kuandaa mwongozo huo kwani ni ishara ya matokeo ya ushirikiano wa taasisi hizo katika kupatia ufumbuzi wa changamoto za kimazingira.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kituo cha Sayansi na Mazingira cha Nchini India (CSE), Nivit Yadav amesema Tanzania ni nchi ya tatu katika Bara la Afrika yenye kasi kubwa ya ongezeko la idadi ya watu na nchi ya pili kwa Mataifa ya Afrika Mashariki kuwa na kasi ya ukuaji wa sekta ya ujenzi, hivyo suala la tathmini ya miradi ya ujenzi ni jambo muhimu linalopaswa kupewa kipaumbele katika uhifadhi na usimamizi wa mazingira.

Amesema Sheria ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004 imeanisha vipaumbele mbalimbali vya utekelezaji wa Sheria hiyo ikiwemo kanuni na miongozo ya utekelezaji ya ushirikiano baina ya Serikali ikiwemo NEMC na CSE.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Dkt. Samwel Gwamaka amesema kwa muda mrefu kumekuwepo na changamoto ya usimamizi wa Tathmini ya Athari kwa Mazingira kupitia maandiko ya miradi mbalimbali yanayowasilishwa kwa ajili ya utoaji wa vibali vya mazingira.

“Awali wataalamu wetu hawakuwa na mwongozo wa maandiko ya tathmini ya miradi ya athari za mazingira ambayo inakidhi matakwa ya Sheria ya Usimamizi wa Mazingira na kanuni zake, baada ya uzinduzi huu sasa wataalamu elekezi wa mazingira na wadau watakuwa na mwongozo wa uandaaji wa maandiko kwa kuzingatia viwango na ubora unaohitajika” amesema Dkt. Gwamaka