π—ͺπ—”π—­π—œπ—₯π—œ 𝗔𝗦𝗛𝗔𝗧𝗨 π—žπ—œπ—π—”π—π—œ π—”π—œπ—§π—”π—žπ—” π— π—˜π—‘π—˜π—π—œπ— π—˜π—‘π—§π—œ 𝗬𝗔 𝗕𝗔π—₯𝗔𝗭𝗔 π—žπ—¨π—¦π—œπ— π—”π— π—œπ—” π—¨π—§π—˜π—žπ—˜π—Ÿπ—˜π—­π—”π—π—œ π—ͺ𝗔 π— π—”π—π—¨π—žπ—¨π— π—¨ π—žπ—ͺ𝗔 π—¨π—”π——π—œπ—Ÿπ—œπ—™π—¨


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Ashatu Kijaji (Mb) ameitaka Menejimenti ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kusimamia kwa uadilifu utekelezaji wa majukumu waliyopewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa niaba ya Watanzania.

Ameyasema hayo alipozuru ofisi za Baraza zilizopo Dar es salaam na kuzungumza na Menejimenti hiyo katika ziara yake ya kwanza ya kikazi mara baada ya kukasimiwa madaraka hayo.

Amesema Viongozi hao wamepewa nafasi na kuaminiwa na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kulitumikia Taifa katika misingi ya uadilifu na weledi na katika misingi ya Sheria ili kuhifadhi na kusimamia Mazingira kwa maendeleo endelevu ya Taifa hivyo hawana budi kuzingatia hayo.

β€œSisi ndio tumepewa dhamana ya kusimamia Mazingira na ndio uhai wa Taifa letu hatuwezi kucheza na suala la Mazingira naomba kila mmoja afanye tathmini ya nafasi aliyopewa kama anaitendea haki kwa uadilifu na ninaamini watumishi wote tuliopo hapa ni wazuri na uzuri wetu upo kwenye utekelezaji wa majukumu tuliyopewa na Mheshimiwa Rais kwa niaba ya Watanzania” amesema Waziri Ashatu

Naye Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis alipozungumza amelipongeza Baraza kwa kuweka kipaumbele utekelezaji wa majukumu yake kwa misingi ya Sheria za Usimamizi wa Mazingira na Utekelezaji wa sheria hizo.

Aidha Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Bw. Abdallah Mitawi amesisitiza kuwa Baraza ni jicho au Taasisi nyeti iliyopo chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais inayosimamia utunzaji na uhifadhi wa Mazingira hivyo yapaswa kutekeleza majukumu yake kwa misingi ya Sheria itakayoleta tija kwa Taifa la Tanzania.

Kadhalika Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Profesa Esnat Chaggu alipozungumza amesema Bodi ya Wakurugenzi inaahidi kutoa ushirikiano wa dhati kwa Waziri Ashatu Kijaji, Baraza na wadau wote wa Mazingira ili kuleta matokeo chanya kwa Taifa.

Katika hatua nyingine Mkurugenzi wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Dkt. Immaculate Sware Semesi ameahidi ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya Baraza na utendaji mzuri kwa Waziri Kijaji ili kufikia malengo kusudiwa kwa maendeleo endelevu ya Mazingira.

β€œMheshimiwa Waziri Tunakuahidi ushirikiano na utendaji mzuri wa majukumu tuliyopewa na Taasisi hii inayogusa Sekta na ngazi zote za mtu yule aliyegusa ardhi au maji kiujumla ni Mazingira” amesema Dkt. Semesi.